Monday, November 26, 2012

North Mara na hatima za familia zilizoumizwa kwa risasi


North Mara na hatima za familia zilizoumizwa kwa risasi


Mkazi wa Kijiji cha Matongo, wilayani Tarime, Mwikwabe Mwita ni mmoja wa watu walioathirika baada ya kutumia maji yanayodaiwa kuwa na sumu kutoka Mto Mara.
Kwa ufupi
“Nakufa hivi hivi, najiona, nateswa na serikali yangu mimi kama kweli Mungu yupo basi damu yetu itatoa majibu, serikali tuliyoichagua ndiyo inatufanyia hivi, nimesema mengi naomba leo niishie hapo,” anasema kisha anakaa kimya.

0
Ukipita karibu na mgodi wa North Mara, utaona nyumba nyingi zimejengwa kwa nyasi au miti na kuezekwa kwa nyasi na nyingine kwa bati. Lakini siyo nyumba zote zimejengwa kwa miti na nyasi, chache zimejengwa kwa matofali na kuezekwa kwa bati.


Mgodi wa North Mara upo katika Kata ya Kemambo na Matongo, Wilaya ya Tarime, mkoani Mara ambako tumekuwa tukisikia kutokea kwa visa vingi vya kuuawawa kwa watu mbalimbali wanaoishi kuzunguka mgodi huo.
Watu hao hasa vijana wamekuwa wakiuawa na polisi wanapoingia kwenye mgodi huo kuchukua mchanga ambao wanauchekecha na kupata dhahabu.
Taarifa zinabainisha kwamba tangu mwaka 2009 mpaka sasa watu 35  wamepoteza maisha kwenye mgodi huo  na wengine kujeruhiwa baada ya kupigwa risasi na askari polisi kwa kushirikiana na walinzi wa kampuni ya African Barrick Gold North Mara.
Mwekezaji North Mara aondolewe
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Tarime na Rorya, Justus Kamugisha anasema njia ya kuzuia wananchi wasipoteze maisha ni kuwahamisha wananchi wanaoishi kuzunguka mgodi huo au wamiliki wa mgodi huo ambao wamekuwa chanzo cha kuuawawa kwa raia.
“Maamuzi magumu yanatakiwa kuchukuliwa, kwanza kuhamisha wananchi ama mwekezaji ahamishwe ili  wananchi wachimbe dhahabu wenyewe kama zamani,” anabainisha Kamanda Kamugisha.
Kamanda huyo anafafanua kwamba  jambo moja kati ya hayo mawili yanapaswa yafanyiwe kazi kwa lengo la  kuzuia matukio ya mauaji na watu kujeruiwa kwa risasi.
Kamanda huyo anasema mgodi kuwapo kwenye makazi ya watu ni hatari kubwa kwa kuwa wakati wanapowathibiti wahalifu wamekuwa wakikimbilia kwenye makazi ya watu.
Anasema hakuna suluhisho zaidi ya hilo kwa kuwa watu wanaoishi karibu na mgodi huo wanaamini kwamba ni mali yao.
Kamanda huyo anasema kutokana na imani hiyo wananchi wamekuwa wakivamia mgodi kwa lengo la kuchukua mchanga na kukutana na mtutu wa bunduki, na kupoteza maisha.
Waziri anasemaje
Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani ambaye ni Waziri wa Ulinzi, Vuai Nahodha anasema kampuni hiyo inapaswa kuajiri askari wa kutosha ili polisi wasiingie kwenye kashfa za kuwaua raia.
“Tumetoa miezi mitatu kwa kampuni kuajiri walinzi wake, polisi watabaki na jukumu la ulinzi wa kawaida, nadhani kwa kufanya hivyo kashfa za polisi kuua ama kujeruhi raia zitapungua kabisa,”anasema Nahodha.
Pia Nahodha amewashauri viongozi wa mgodi huo kuwaletea wananchi maendeleo na kutoa ajira za kutosha kwa wakazi wa maeneo hayo.
Polisi wamekuwa wakipelekwa kwa wingi kulinda mgodi huo huku baadhi ya wakidokeza posho kubwa wanazolipwa na maofisa wa mgodi huo ni kichocheo kikubwa cha kukimbilia kulinda mgodi huo.
Wachimbaji wadogo wadai serikali haina mpango wa kumaliza mauaji dhidi ya raia kwa kuwa ingetaka kufanya hivyo ingewaita na kujadiliana jinsi ya kutatua tatizo hilo.
Dhahabu na mauaji ya kikatili
Mwenyekiti wa ushirika wa wachimbaji wadogo wadogo wilayani Tarime, Daud Makona anasema mauaji ya kikatili yanayoendelea katika mgodi huo ni mpango wa serikali baada ya kushindwa kuendeleza eneo la wachimbaji wadogo la Msege na kusajili ushirika huo tangu mwaka 2010.
“Serikali haiwezi kukwepa mauaji yanayoendelea mgodini kwa sababu kama maeneo ya  wachimbaji wadogo wadogo yangeendelezwa, mgodi huo usingevamiwa,”anasema Makona.
Mwenyekiti huyo alishangazwa na kauli ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye aliwashauri wachimbaji wadogo wa Mgusu, mkoani Geita waunde ushirika ili  wasaidiwe wakati wao wameunda, lakini mpaka sasa ushirika huo haujasajiliwa.
“Hakuna waziri ama kiongozi aliyekuja na kukutana na wachimbaji wadogo, wote wanaishia mgodini, hakuna dhamira ya kweli ya kukomesha mauaji,”anasema.
Makona anasema Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, William Ngeleja alitoa ahadi nyingi za kuwasaidia wachimbaji wadogo, lakini hazijatekelezwa wakati Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Massele amefika Nyamongo mara mbili ndani ya miezi mitatu, na Waziri wa wizara hiyo Profesa Sospeter Muhongo aliishia Tarime, wote hawakukutana na wachimbaji wadogo.
Serikali yetu ni sikivu?
Mkazi wa Kitongoji cha Kwinyunyi, Kijiji cha Matongo, Esther Mugusuhi (63) ambaye ni miongoni mwa waathirika aliyetumia maji yenye sumu katika Mto Mara, anasema anasema serikali inapaswa kutoa taarifa ni kwa kiwango gani maji hayo yamewaathiri wananchi na jinsi ya kubaini maji yenye sumu hiyo.
“Vyanzo vya maji vimeharibiwa watu wanakufa, lakini mpaka sasa hatujaelezwa ni kwa kiwango gani tumeathirika,  wanatuambia serikali sikivu, huku ikiwa kimya,  haisikii na wala
haisemi lolote,”anasema.
Matokeo ya madhara wanayopata yamekuwa yakiamsha hasira kwa vijana ambao wamekuwa wakipambana askari wanaolinda mgodi huo.
Mkazi wa Kitongoji cha Lamboni katika Kijiji cha Kewanja, Mwikwabe Mwita (69) anasema anasubiri kufa, lakini hajui hatima ya familia yake.

“Nakufa hivi hivi, najiona, nateswa na serikali yangu mimi kama kweli Mungu yupo basi damu yetu itatoa majibu, serikali tuliyoichagua ndiyo inatufanyia hivi, nimesema mengi naomba leo niishie hapo,” anasema kisha anakaa kimya.
Mtafiti kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Onesmo Ole Ngurumwa anasema zaidi ya watu 35 wameuawa na jeshi la polisi katika mgodi wa African Barrick North Mara tangu mwaka 2009.
Anasema matatizo yanayowakumba wakazi hao ni mengi yakiwamo ya kutumia maji yenye sumu kutoka katika mgodi huo, kuuawa, kubakwa, kujeruhiwa, na kuongezeka kwa yatima.
Hivi karibuni Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Maselle aliwathibitishia wafanyakazi wa mgodi huo kwamba utauzwa kwa kampuni ya Kichina na kuahidi watasimamia utekelezaji wa ahadi zake na kuweka mazingira mazuri kwa jamii ili kuepuka matukio kama hayo.
Mwaka 2009 kamati tatu za bunge ya afya, mazingira na madini chini ya
mbunge Job Ndugai zilifanya ziara mgodini hapo na kuunda tusk force kushughulikia madhara yaliowapata wakazi wa eneo baada ya kutumia maji yenye sumu, lakini mpaka sasa kamati hizo hazijatoa taarifa za  wazi kwa wananchi.
Licha ya wakazi wa Kata ya Kibasuka kujitokeza mbele ya kamati tatu za
wabunge wakiwa wameathirika na kukabidhi majina ya watu waliofariki dunia na mifugo, serikali haijawahi kutoa taarifa ya uchunguzi uliofanywa madhara yaliowapata watu na mifugo.


No comments:

Post a Comment