Tuesday, December 18, 2012

KUWEKEA NDOA YAKO MSINGI MZURI(3);

KUWEKEA NDOA YAKO MSINGI MZURI(3);
KUFAANA.
Ukifahamu mambo yote hayo yanayotakiwa na mwili, akili na roho, Je! Unajua kama mtu unayetazamia kuoana naye anayafahamu vilevile? Haikupasi ujue tu mambo ambayo wewe peke yako unataka ili uwe na furaha katika ndoa, bali yakupasa vilevile ufahamu na yale ya mwenzako. Bila shaka wataka mwenzako awe na furaha vilevile. Huzuni ya mmoja itakuwa huzuni ya nyote wawili.
Ndoa nyingi zitakuwa na mwisho wenye huzuni au talaka kwa sababu za kukosa kufaana(kutopatana). Kutofaana ni neno kubwa, lakini linakuwa kubwa hata zaidi katika ndoa. Ikiwa watu wawili hawafaani kukaa pamoja, maisha yanaweza kuwa yenye matata. Hali hiyo inakumbusha mpango wa sheria ya Musa ambayo kwa sababu ya rehema ilikataza kufunga pamoja wanyama wawili wenye mwili na nguvu tofauti katika nira moja, kwa sababu kufanya hivyo kungefanyiza matata(Kumbukumbu la torati 22:10)Ndivyo walivyo mwanamume na mwanamke wasio faana lakini wanaofungwa katika ndoa. Ikiwa waume na wake wanakuwa na mapendezi tofauti , rafiki tofauti, na tafrija tofauti, na kushiriki pamoja mambo machache, vifungo vya ndoa vinapata matata makubwa.
“Pasipo mazungumzo ya siri, mipango inavunjika,” ndiyo Biblia inavyotuambia. (Mithali 15:22) Je!mambo yanayofaa yamezungumzwa wakati wa kufikiria ndoa? Itaamua mahali mtakakoishi na kiasi cha fedha zitakazokuwa zikipatikana ili mtimize mambo yanayofaa mnayotaka. Ni nani atakayekuwa akifanya mipango ya matumizi ya fedha? Je! Kuna lazima ya mke kufanya kazi, na je! Inafaa? Uhusiano (hali) pamoja na wakwe utakuwaje, sana sana wazazi wa mume na wale wa mke? Kila mmoja anaonaje ngono, watoto na kulea watoto? Je! Mmoja anataka kumtawala mwenzake, au huruma ndiyo itakayoongoza uhusiano huo?
Je! Maulizo hayo yote na mengine vilevile, yaweza kuzungumzwa kwa utulivu na kwa busara, na kumalizwa kwa njia ambayo nyote wawili mwaweza kuishi kwa raha? Je! Mwaweza kupata magumu na kuyamaliza pamoja, na kuendelea kupashana habari siku zote? Hiyo ndiyo njia ya maisha ya ndoa inayofanikiwa.
Kwa kawaida kufaana zaidi kunakuwako kati ya watu wawili wanaopatana hali za maisha. Kitabu cha Aid to bible understanding, ukurasa 1114, kinaeleza hivi juu ya ndoa katika nyakati za biblia: “Inaonekana kwamba desturi ya watu wote ilikuwa ile ya mwanamume kuoa katika watu wa ukoo au katika kabila lake mwenyewe.Kanuni hiyo inaonyeshwa na maneno ya Labani aliyomwambia Yakobo: ‘Afadhali nikupe wewe (binti yangu) kuliko kumpa mtu mwingine.’- Mwanzo 29:19 sana sana desturi hiyo ilifuatwa na waabudu wa Yehova, kama Ibrahimu alivyoonyesha kwa kumpeleka mjumbe aende kwa watu wa ukoo wake katika nchi yake mwenyewe akamtafutie Isaka mwanawe mke badala ya kuchukua mmojawapo wa binti za Wakaanani ambao alikuwa akikaa kati yao.(Mwanzo 24:3,4)”
Lakini, hiyo haina maana ya kwamba yafaa mtu leo aoe au aolewe na mtu wa ukoo wake wa karibu sana, kwa maana hiyo ingeweza kuleta magumu na kufanya watoto wazaliwe wakiwa na kasoro Fulani. Lakini hali za jamaa moja zinahusu sana kanuni za watu. Wakati wa utoto na ujana, mwenendo wa mtu na maoni yake yanaongozwa na hali jamaa. Watu wawili wanapokuwa na hali moja ya maisha, wanaona kuwa vyepesi zaidi kupatana. Lakini, watu wasio wa hali moja za maisha na ukoo mmoja wanaweza vilevile kufanya mageuzo mema katika ndoa, sana sana wote wawili wakiwa wamekomaa moyoni.
Kwa wazi, inafaa sana ikiwa unaweza kujua habari za jamaa ya mtu unayetazamia kuoana naye. Chunguza vilevile ujue uhusiano wake na jamaa hiyo na wazazi na ndugu na dada zake kama wapo. Anatendeaje wazee, au anapatanaje na watoto wdogo?
Ijapokuwa unakuwa mwangalifu katika mambo yote, yakupasa bado ukumbuke hili: Watu wawili hawawezi kufaana kabisa kabisa hata. Wote wawili watakuwa na makosa Fulani. Labda wanaweza kujua machache kabla ya kuoana; na mengine watayajua baadaye. Halafu?
Si makosa yenyewe yanayofanya ndoa zisifanikiwe, bali ni namna hao wawili wanavyoyaona. Unaweza kuona kwamba mema yanashinda mabaya, au unakaza fikra juu ya mabaya na kuyarudia ridia? Je! Uko tayari kukubali na kukumbuka kwamba mwenzako anaweza kufanya makosa, kama vile wewe unavyotaka utendewe? Mtume Petro alisema, “Upendo unafunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8) Je! Unampenda namna hiyo mtu Yule unayemfikiria kuoana naye? Ikiwa sivyo, afadhali usioane na mtu huyo?

No comments:

Post a Comment