KUWEKEA
NDOA YAKO MSINGI MZURI(3);
KUFAANA.
Ukifahamu mambo yote hayo yanayotakiwa
na mwili, akili na roho, Je! Unajua kama mtu unayetazamia kuoana naye
anayafahamu vilevile? Haikupasi ujue tu mambo ambayo wewe peke yako
unataka ili uwe na furaha katika ndoa, bali yakupasa vilevile ufahamu
na yale ya mwenzako. Bila shaka wataka mwenzako awe na furaha
vilevile. Huzuni ya mmoja itakuwa huzuni ya nyote wawili.
Ndoa nyingi zitakuwa na mwisho wenye
huzuni au talaka kwa sababu za kukosa kufaana(kutopatana). Kutofaana
ni neno kubwa, lakini linakuwa kubwa hata zaidi katika ndoa. Ikiwa
watu wawili hawafaani kukaa pamoja, maisha yanaweza kuwa yenye
matata. Hali hiyo inakumbusha mpango wa sheria ya Musa ambayo kwa
sababu ya rehema ilikataza kufunga pamoja wanyama wawili wenye mwili
na nguvu tofauti katika nira moja, kwa sababu kufanya hivyo
kungefanyiza matata(Kumbukumbu la torati 22:10)Ndivyo walivyo
mwanamume na mwanamke wasio faana lakini wanaofungwa katika ndoa.
Ikiwa waume na wake wanakuwa na mapendezi tofauti , rafiki tofauti,
na tafrija tofauti, na kushiriki pamoja mambo machache, vifungo vya
ndoa vinapata matata makubwa.
“Pasipo mazungumzo ya siri, mipango
inavunjika,” ndiyo Biblia inavyotuambia. (Mithali 15:22) Je!mambo
yanayofaa yamezungumzwa wakati wa kufikiria ndoa? Itaamua mahali
mtakakoishi na kiasi cha fedha zitakazokuwa zikipatikana ili mtimize
mambo yanayofaa mnayotaka. Ni nani atakayekuwa akifanya mipango ya
matumizi ya fedha? Je! Kuna lazima ya mke kufanya kazi, na je!
Inafaa? Uhusiano (hali) pamoja na wakwe utakuwaje, sana sana wazazi
wa mume na wale wa mke? Kila mmoja anaonaje ngono, watoto na kulea
watoto? Je! Mmoja anataka kumtawala mwenzake, au huruma ndiyo
itakayoongoza uhusiano huo?
Je! Maulizo hayo yote na mengine
vilevile, yaweza kuzungumzwa kwa utulivu na kwa busara, na kumalizwa
kwa njia ambayo nyote wawili mwaweza kuishi kwa raha? Je! Mwaweza
kupata magumu na kuyamaliza pamoja, na kuendelea kupashana habari
siku zote? Hiyo ndiyo njia ya maisha ya ndoa inayofanikiwa.
Kwa kawaida kufaana zaidi kunakuwako
kati ya watu wawili wanaopatana hali za maisha. Kitabu cha Aid to
bible understanding, ukurasa 1114, kinaeleza hivi juu ya ndoa katika
nyakati za biblia: “Inaonekana kwamba desturi ya watu wote ilikuwa
ile ya mwanamume kuoa katika watu wa ukoo au katika kabila lake
mwenyewe.Kanuni hiyo inaonyeshwa na maneno ya Labani aliyomwambia
Yakobo: ‘Afadhali nikupe wewe (binti yangu) kuliko kumpa mtu
mwingine.’- Mwanzo 29:19 sana sana desturi hiyo ilifuatwa na
waabudu wa Yehova, kama Ibrahimu alivyoonyesha kwa kumpeleka mjumbe
aende kwa watu wa ukoo wake katika nchi yake mwenyewe akamtafutie
Isaka mwanawe mke badala ya kuchukua mmojawapo wa binti za Wakaanani
ambao alikuwa akikaa kati yao.(Mwanzo 24:3,4)”
Lakini, hiyo haina maana ya kwamba
yafaa mtu leo aoe au aolewe na mtu wa ukoo wake wa karibu sana, kwa
maana hiyo ingeweza kuleta magumu na kufanya watoto wazaliwe wakiwa
na kasoro Fulani. Lakini hali za jamaa moja zinahusu sana kanuni za
watu. Wakati wa utoto na ujana, mwenendo wa mtu na maoni yake
yanaongozwa na hali jamaa. Watu wawili wanapokuwa na hali moja ya
maisha, wanaona kuwa vyepesi zaidi kupatana. Lakini, watu wasio wa
hali moja za maisha na ukoo mmoja wanaweza vilevile kufanya mageuzo
mema katika ndoa, sana sana wote wawili wakiwa wamekomaa moyoni.
Kwa wazi, inafaa sana ikiwa unaweza
kujua habari za jamaa ya mtu unayetazamia kuoana naye. Chunguza
vilevile ujue uhusiano wake na jamaa hiyo na wazazi na ndugu na dada
zake kama wapo. Anatendeaje wazee, au anapatanaje na watoto wdogo?
Ijapokuwa unakuwa mwangalifu katika
mambo yote, yakupasa bado ukumbuke hili: Watu wawili hawawezi kufaana
kabisa kabisa hata. Wote wawili watakuwa na makosa Fulani. Labda
wanaweza kujua machache kabla ya kuoana; na mengine watayajua
baadaye. Halafu?
Si makosa yenyewe yanayofanya ndoa
zisifanikiwe, bali ni namna hao wawili wanavyoyaona. Unaweza kuona
kwamba mema yanashinda mabaya, au unakaza fikra juu ya mabaya na
kuyarudia ridia? Je! Uko tayari kukubali na kukumbuka kwamba mwenzako
anaweza kufanya makosa, kama vile wewe unavyotaka utendewe? Mtume
Petro alisema, “Upendo unafunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8)
Je! Unampenda namna hiyo mtu Yule unayemfikiria kuoana naye? Ikiwa
sivyo, afadhali usioane na mtu huyo?
No comments:
Post a Comment