Ingawa
sisi si wakamilifu mbele za Mungu na tunafanya makosa lakini tunaweza
kufanikiwa maishani. Kwa kusoma maandiko matakatifu (Biblia) inaweza kukusaidia
ufikie lengo hilo,
kwani kwa kusoma tunapata hekima ya Mungu. “Lakini hekima itokayo juu, kwanza
ni safi, tena
ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na
matunda mema, haina fitina, haina unafiki.” Yakobo 3:17.
1. KUWA NA MTAZAMO UNAOFAA KUHUSU PESA.
“Maana
shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali
wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani na kujichoma kwa maumivu mengi” (I
Timotheo 6:10). Siku zote tatizo sio kuwa na pesa maana tunahitaji pesa ili
kukidhi kupata mahitaji yetu ya kila siku na kutunza familia zetu pia.
Tatizo lililopo
ni KUPENDA PESA. Maana katika kupenda pesa kwaweza kumfanya mtu kuanza kuiabudu
pesa kama ndio Mungu wake na kuanza kusahau
kumwabudu MUNGU aliyemuumba.
Watu ambao
hutafuta kuwa matajiri ili wapate mafanikio nikimaanisha KUPENDA PESA wengi wao
ingawa sio wote wamejikuta katika maumivu makali, Maana katika harakati zao za
kutafuta pesa wengine kwa njia za kufanya Ufisadi kwa kuiba mali za uma, kuwadhulumu
wajane, Yatima na hata wengine kwa kuwakata viungo walemavu wa ngozi (albino),
wamekosa kuwa na Amani maishani mwao hivyo kukosa usingizi sit u kwa sababu ya
kazi nyingi bali kwa kuwa na wasiwasi mioyoni mwao maana wamejitengenezea
maadui katika familia zao, na hata miongoni mwa marafiki zao. “Usingizi wake
kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi. Lakini
kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi”(Mhubiri 5:12).
Zaidi ya kuwa bwana mkatili, kupenda
pesa ni bwana mdanganyifu (Marko 4:19). Maana yake ni kwamba utajiri humwahidi
mtu kupata furaha lakini haufanyi hivyo. Baada yake umfanya mtu atamani utajiri
zaidi. Ebu soma nami katika kitabu cha Mhubiri 5:10. “Apendaye fedha hatashiba
fedha, wala apendaye wingi hatashiba maongeo. Hayo pia ni ubatili”.
Kifupi ni kwamba mtu anayependa pesa
sana anajiumiza tu.Anavunjika moyo, anakatishwa
tama au hata kujihusisha katika uhalifu Mithali 28:20 “Wasio haki wainukapo,
wanadamu hujificha; Bali waangamiapo, wenye
haki huongezeka”.
Ukarimu, Usafi wa maadili, Mahusiano
mazuri pamoja na Mungu, Upendo na kuwa tayari kusamehe hayo ni mambo yanayoleta
furaha na mafanikio maishani.
2. KUWA NA ROHO YA UKARIMU.
“Katika
mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge,
na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa
kuliko kupokea”. Unapokuwa na Roho ya Ukarimu kwa watu wote walio na uhitaji na
wasio nao unakuwa na furaha ya kudumu moyoni mwako maana unapowatendea mojawapo
ya hao unakuwa unamtendea Mungu.
Mtafiti
mmoja mara baada ya kufanya uchunguzi wa muda mrefu kuhusu afya, furaha, na
kutokuwa na ubinafsi, mtafiti alibaini kwamba kutokuwa na ubinafsi na
kuwasaidia wengine kunahusianishwa na maisha marefu, afya nzuri kimwili, kiakili,
kijamii na kiroho lakini pia husaidia kupunguza kupatwa na kushuka kwa moyo.
Lakini
pia watu wenye roho ya ukarimuhawapungukiwi na kitu chochote maishani. “Nafsi
ya mtu mkarimu itawandishwa, Anyweshaye atanyweshwa mwenyewe”. (Mithali 11:25).
Hii inamaanisha kwamba wale wote
wanaofanya ukarimu toka moyoni na sio wale wanaojifanya ni wakarimu ili watu
wawaone kuwa ni wakarimu huku wakitarajia siku moja na wao watawalipa fadhila
zao. Sasa kwa wale walio na ukarimu wa moyoni sadaka zao hizo zinampendeza Mungu
sana (Waebrania
13:16)
3. SAMEHE KWA AJILI YA YESU.
Siku
hizi watu wengi pale wanapoombwa msamaha
na wale waliowakosea usema mioyoni mwao kuwa NIMEKUSAMEHE LAKINI SITAKUSAHAU.
Huo utakuwa ni msamaha wa kinafiki. Ebu niwaeleze jambo moja lililowahi tokea huko
Afrika ya kusini enzi ubaguzi wa rangi mama mmoja aliyekuwa na na kijana wake
ambaye kutokana na ukandamizaji wakati huo mtoto wake alitiwa mikononi mwa
polisi kasha kutokana na mateso huko kizuizini alifia huko na mara baada ya
kuundwa kwa tume ya ukweli na maridhiano huko Afrika ya kusini Chini ya Askofu
Desmond Tutu askari polisi mmoja alikutwa na hatia ya kumuua kijana wa mama
huyo, kesi ilipopelekwa mahakamani yule mama akaona hata polisi huyo
atakapokutwa na hatia ya mauaji hawezi kumpata kijana wake, hivyo basi mama
huyo alipoitwa na tume hiyo alieleza kuwa yeye yuko tayari kumsamehe askari
polisihuyo wakati wa enzi za utawala wa makaburu na tena akasema kuwa kuanzia
wakati huo yeye ndiye atakuwa sawa na kijana wake. Ni msamaha wa wa namna ya
pekee sana na wa nadra sana mioyoni mwa wale waliopotelewa na
wapendwa , au wazazi wao.
Katika
ripoti moja ya Gazeti la The Gazette la Montreal,
Canada inasema
kwamba “Katika uchunguzi uliofanyiwa watu zaidi ya 4600 wenye umri ya kati ya
miaka 18 hadi 30”,wachunguzi waligundua kwamba uhasama, kukata tama, na
kutokuwa na fadhili hufanya mapafu yawe mabovu. Kwa kweli mambo hayo yanaweza
kufanya mapafu ya mtu kuwa mabovu zaidi kuliko ya mvutaji wa sigara.
Kumbe
kusamehe hakufanyi iwe rahisikushughulika na wengine tu bali pia unafaidisha
Afya zetu.
Ili tuweze kusamehe zaidi ebu anza kujichunguza kwamba
je, wakati mwingine huwa hauwakasirishi watu? Unafurahi wanapokusamehe?Kwa hiyo
mbona hauwasamei wengine?. Hata kama kulikuwa na mtu aliyetaka kuiangamiza roho yako kwa uchawi au kwa kukuwekea sumu
kwenye chakula bado tunaambiwa ni sharti tuwarehemu.(Mathayo 18:21-35).
Tambua kuwa
kujizuia sio udhaifu kuliko kulipiza ovu kwa ovu. Ebu soma kitabu cha Mithali
16:32 “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa. Na mtu aitawalaye roho
yake kuliko mtu atekaye mji”.
4. KUISHI KWA KUFUATA KANUNI ZA MUNGU.
“Maagizo
ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya BWANA ni safi, huyatia macho nuru”. (Zaburi 19:8). Kwa
kweli kanuni (sheria) za Mungu zinafaida kubwa sana
kwetu wanadamu maana zinatulinda dhidi ya mazoea mabaya kama
vile kutumia dawa za kulevya, pombe, ukosefu wa maadili na kutazama, kuona au hata kusikiliza habari na picha zenye
kuamsha hisia za ngono. (II Wakorintho 7:1; Wakolosai 3:5) Unapojiingiza katika
mazoea hayo mabaya yanaweza kuleta athari mbaya kama
uharibifu,umaskini, kutoaminiana, kuvunjika kwa familia, matatizo ya kiakili na
kihisia, magonjwa na kifo cha mapema.
Kwa
wale wanaoishi kwa kufuata kanuni za Mungu wanakuwa na mahusiano mazuri,
wanajiheshimu, na kuwa na Amani ya akili. Katika kitabu cha Isaya 48:17,18
inasema hivi “Bwana mkombozi wako, mtakatifu wa Israel asema hivi; mimi ni BWANA,
Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida nikuongozaye kwa njia ikupasayo
kuifuata Laiti ungalisikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingalikuwa kama mto
wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari;”
5. KUONYESHA UPENDO USIO NA UBINAFSI.
“Na
kwa habari ya vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu; Twajua ya kuwa sisi sote
tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga”.(I Wakorintho 8:1)
Tunachokiona
hapa ni kuwa Upendo hujenga, Huweza kujenga mahusiano mazuri kati ya mtu na mtu
pamoja na kuleta ushirikiano toka jamii moja na hadi nyingine. Na maana halisi
ya Upendo ni kujitoa wewe mwenyewe bila ya uhakika kuwa upendo wako utarejeshwa
. Kwa maana hiyo basi Upendo ni tendo la Imani
wala halihitaji kurudishwa.
“Tena
nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na Imani
timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama
sina Upendo, si kitu mimi. Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu;
upendo hautakabali; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake;
hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na
kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote”. (I
Wakorintho 13:2,4-7)
Upendo
unaotajwa hapa si ule wa kimahaba ambao una mahali pake panapofaa. Badala yake
ni upendo unaodumu ambao unaongozwa na kanuni za Mungu. Isitoshe, mtu
haonyeshwi tu upendo huo bali anauonyesha kwa matendo.
Kwa
wazazi, Upendo unamaanisha kuwa na hisia
nyororo kuwaelekea watoto wao na kuwapa mwongozo ulio wazi unaotegemea Biblia
kuhusu maadili na tabia nyingine. Watoto wanaolelewa katika mazingira kama hayo hujihisi salama,Wanapendwa, na kuthaminiwa
wakiwa sehemu ya familia iliyo imara.
Kwa
wenzi walio na matatizo katika ndoa yao
wanaamua kusoma pamoja maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Marko 10:9
yanayosema “Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe”. Sasa,
lazima wajichunguze mioyo yao.
Je wanashangilia pamoja na kweli za biblia? Je wataiona na kuitendea ndoa kama
kitu kitakatifu, kama vile Mungu anavyoiona?
Je wako tayari kujitahidi kutatua matatizo yao kwa upendo? Kwa kufanya hivyo wanaweza
kufanya ndoa yao
ifanikiwe na kuanza upya kufurahia Upendo ule wa mwanzo.
6. TAMBUA UHITAJI WAKO WA KIROHO.
“Heri walio maskini wa roho, Maana ufalme wa mbinguni ni wao” (Mathayo
5:3). Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, tofauti na
wanyama wanadamu wana uwezo wa kuthamini mambo ya kiroho. Tutatambua uhitaji
wetu wa kiroho pale tutakapokuwa watu wa kutaka kujifunza maneno ya Mungu kila
mara na kuomba zaidi, ndipo yule roho atakapomwagwa kwa wingi sana ndani yetu. Kumwagwa kwa roho wa Mungu
kwa wingi kutaamsha hari ya kuifanya kazi ya Mungu kwa nguvu zote, akili zote
na uwezo wote kisha twende nyumbani kuishi milele.
“Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na
Yesu kristo uliyemtuma” (Yohana 17:3). Kumbe uzima wa milele unapatikana pale
tunapomjua Mungu na kuitenda kazi yake hapa duniani.
No comments:
Post a Comment