ALBINO NAYE NI MTU KAMA WENGINE.
Neno Albino linamaanisha mtu
mweupe, linatokana na neon la lugha ya kilatini –albus-lino maanisha “-eupe”. Kuanzia karne ya 17 neno Albino
limekuwa likitumika katika kueleza hali ya kundi la viumbe hai (watu, wanyama
na hata mimea) ambao wana upungufu au ukosefu wa rangikatika ngozi, macho na
nywele. Kwa binadamu ni bora kutumia maneno “Watu wanaoishi na ualbino kwani
itamaanisha kuwa ni watu kama wengine
ila wanaishi na hali tofauti ya “ualbino”.
Lugha inajenga dhana na kuunda
hali ya ukweli/uhalisi. Kwa sababu hiyo ni lazima tuache kutumia maneno “zeruzeru”. Neno hili linamaanisha sifuri
mara mbili au mtu asiye na thamani. Utumiaji
wa neno hili ni dharau ya utu na
kulaumu watu wanaoishi na ualbino kama kosa lao.
Albino wana ngozi nyeupe, nywele
nyeupe au nyekundu na macho ya kijivu au ya bluu. Ngozi yao ni nyeupe zaidi
kuliko ndugu zao wa familia moja au watu wa jamii yake ambao hawana hali ya
ualbino. Ngozi hii inaonekana zaidi kuwa nyeupe katika familia za watu weusi,
ingawaje, ualbino hutokea kwa watu wa kila taifa, rangi, kabilana dini. Albino
wako katika mabara yote ulimwenguni.
Je ualbino unasababishwa na nini? Watu wenye ualbino
hawana uwezo kabisa au wana uwezo mdogo wa kuwa na rangi kwenye ngozi zao,
nywele na macho. Rangi hii huitwa
“melanini”. Rangi ya ngozi itategemeana na kiasi cha melanini kilichopo.
Hali ya kuzalisha melanini imekaa katika vinasaba vyetu. Kama vinasaba vya
kutoa melanini havipo au vimebadilishwa madhara yake ni ukosefu au upungufu wa
rangi. Kwa hiyo hali ya ualbino ni ya kurithi. Inaweza kurithishwa kutoka kwa
wazazi kwenda kwa mtoto.
Je ualbino unarithiwa vipi?
Watoto wengi
wanaozaliwa na ualbino, wazazi wao wana rangi ya ngozi, nywele na macho
inayofanana na watu wa kabila /asili yao. Mwili wa kila mwanadamu una seti
mbili za vinasaba (moja hutoka kwa mama na moja hutoka kwa baba). Mtu anaweza
kuwa na rangi ya asili ya kawaida lakini akawa na kinasaba cha ualbino. Kama
mtuana kinasaba kimoja cha rangi ya asili na kimoja cha ualbinoatakuwa na taarifa za vinasaba vya kutosha
kutengeneza rangi ya asili. Kinasaba cha
ualbino ni seli dhoofu haiwezi peke yake kuonyesha ualbino mpaka mtu awe nazo
mbili kwa pamoja.
Kama wazazi wote wawili wana
vinasaba vya ualbino na wote hawaonyeshi ualbino, kuna uwezekano wa kupata
mtoto Albino kati ya mmoja katika wanne kwa kila mimba.
Ni wanadamu tu pekee ndiyo
wameathiriwa na ualbino?
Hapana. Ualbino ni
hali inayoweza kutokea kwa wanadamu na wanyama wa kundi la mamalia. Tembo weupe
wa India hujulikana sana na walithaminiwa sana katika mahakama ya mfalme ,
vilevile chui, twiga na samba weupe ambao sasa wanafurahiwa sana kwenye bustani
za wanyama na mbuga za wanyamapori.
Hapa Tanzania inakisiwa kuwa kuna
Albino wapatao zaidi ya elfu kumi hivi, na kwa wingi wanapatikana katika maeneo
ya mikoa ya kanda ya ziwa –Tanzania. Inakisiwa kwa mujibu wa tafiti katika nchi
nyingine kama Nigeria na Afrika kusini kuwa kuna mtu 1 kati ya 4,000-5,000 ni
albino na idadi hii ni kubwa sana ukilinganisha na Ulaya au Marekani
ambapo ni wastani wa mtu 1 kati ya watu 15,000-20,000 hivi.
Watu wanaoishi na ualbino
wanafanana wote? Hapana. Albino
wote hawafanani bali wanatofautiana kufuatana na kiasi cha melanini walicho
nacho wengine hawana kabisa na wengine wanayo kwa kiasi kidogo tu. Wanasayansi
wamegundua aina mbalimbali za ualbino. Kufuatana na aina hizi za ualbino
wengine wana ngozi ya rangi ya kahawia nyepesi na nywele nyeupe, wengine wana
ngozi nyeupe na nywele nyeupe, baadhi wana mabaka meusi machache kwenye ngozi
nyeupe.
Nini matatizo ya macho ya Albino? Mboni katika macho
ya Albino haina pigimenti ya rangi. Kwa hiyo ni rahisi macho yao kuathiriwa na
mwanga. Kwani mboni ndiyo inayolinda jicho la ndani lisipatwe na mwanga mkali.
Vilevile kama mboni inavyolinda jicho dhidi ya mionzi ya jua, inakuwa vigumu
kuona kwa usahihi utofautikatika picha. Kwa hiyo uwezo wa kuona unatiwa mawingu
mawingu. Hivyo basi ni muhimu sana kukwepa inavyowezekana mionzi ya jua na
kulinda macho kwa kuvaa miwani ya jua. Albino mara nyingi hawaoni vizuri na hii
inatofautiana kwa mmoja hadi mwingine. Inawezekana ni kutoona mbali,kutoona
karibu au kuona mawingu mawingu. Matatizo haya hutofautiana katika albino.
Ukweli ni kuwa albino anaweza kushiriki katika michezo mbalimbali, baadhi
wanaweza kuendesha magari na wengi wanaweza kusoma maandishi ya
kawaida.
Kwanini Albino wanawekwa katika
kundi la walemavu?
Ulemavu maana yake
ni hitilafu katika mwili au akili inayomwekea mipaka mtu asiweze kufanikisha
shughuli Fulani katika maisha yake. Albino wanatambuliwa kama watu wenye
ulemavu hasa kwa ajili ya uwezo wao wa kutokuweza kuona vizuri. Dalili za kutokuwa
na uwezo wa kuona vizuri hutofautiana kuanzia wale ambao hawaoni karibu,
wasioweza kuona mbali na wale ambao wanashindwa kuona vizuri au kuona mawingu
mawingu.
Pamoja na matatizo ya kuona,
ngozi ya albino ni rahisi sana kudhurika kwa mionzi ya jua. Hatma yake ikiwa ni
uwezekano mkubwa wa kupata saratani ya ngozi. Hivyo basi kila albino
anashauriwa daima kujikinga dhidi ya mionzi ya jua kwa kuvaa nguo za mikono
mirefu, kuvaakofia pana, kuvaa miwani ya jua na kwa wale wenye uwezo kujipaka
mafuta maalumu yanayosaidia kukinga ngozi dhidi ya mionzi ya jua.
Albino ni watu wa kawaida, je
kisayansi hii ni kweli?
Hii ni kweli
kabisa. Watu wanaoishi na ualbino ni watu wa kawaida kama binadamu wengine wote
na wanaweza kuwa wa aina tofauti kama binadamu wengine. Wanaweza kuwa wadogo au
warefu, wanene au wembamba, warembo au wasio warembo, wenye vipaji au wa
wastani. Wanaweza kuwa na uthubutu au wenye aibu, wachangamfu au jeuri, wenye
tabia ya ushirikiano au wenye tabia ya uhasama.
Kumbuka kuwa utofauti wao upo tu kwenye muonekano wa ukosefu wa
rangi kwenye ngozi, nywele na macho. Wakati umefika jamii kujifunza kuwakubali
albino kama binadamu wengine, wenye hisia, mahitaji, uwezo na wanastahili haki
zote za binadamu kama alivyo mtu mwingine yeyote.
Albino anaweza kuwa na maisha ya
kawaida na yenye mafanikio katika maisha?
Imani iliyojengeka
kwenye jamii kuwa albino wana uwezo mdogo si ya kweli. Ipo mifano mingi ya
watuwalioweza kupata mafanikio katika maisha ambao pia ni albino. Wapo ambao ni
waalimu, wanasayansi, wanasheria, na wengine wapo kwenye siasa na uongozi.
Mwanamuziki wa kimataifa kutoka nchi ya Mali anayeitwa Salif Keita amefikia
mafanikio makubwa sana duniani kote kuanzia bara la Afrika na Ulaya kiasi cha
kuitwa “Sauti ya dhahabu”. Yeye alizaliwa katika familia ya muasisi wa taifa la
Mali Sundiata keita. Hii inadhihirisha
kuwa albino anaweza kuzaliwa katika familia yeyote kuanzia zile za kifalme na
hata familia maskini za wakulima wadogo wadogo.
Je zipo sheria zinazolinda watu
wenye ulemavu hapa Tanzania? Ndiyo zipo sheria
hapa Tanzania zinazowalinda watu wenye ulemavu, Tanzania ilitia saini na
kuridhia mkataba wa kimataifa wa ulinzi, haki na usawa kwa watu wenye ulemavu
mwaka 2006. Kwa kitendo cha kuridhia mkataba huo wa kimataifa Tanzania
imeonyesha nia yake ya kuwalinda na kudumisha haki za watu wenye walemavu. Hata katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ya mwaka 1977(Kama ilvyofanyiwa marekebisho mara kwa mara) inakataza
ubaguzi wa aina yeyote kwa watu wenye ulemavu.
Zipo sheria nyingi zinazolinda
haki na usawa kwa walemavu ambazo zinahusika na sekta mbalimbali kwa mfano;
elimu na mafunzo, ajira(sheria ya watu wenye ulemavu Na.2
ya mwaka 1982, matunzo(kanuni za ajira za watu wenye ulemavu Na. 3 ya mwaka 1985, na ustawi(sheria ya matunzo ya
watu wenye ulemavu Na.3 ya mwaka 1982. Ipo pia sera ya taifa kuhusu
ulemavu ya mwaka 2004(Sheria ya haki na upendeleo kwa watu wenye ulemavu Na.9
ya mwaka 2006, na hii ni kwa
Zanzibar tu.
JE, ZIPO SHERIA ZINAZOLINDA HAKI
ZA ALBINO?
Haki za msingi za
albino zinalindwa chini ya katiba ya nchi pamoja na sheria zinazohusika na
sekta mbalimbali. Sheria hizi zinakataza na kukemea aina zote za ubaguzi kwa
misingi ya rangi, kabila, ulemavu na kadhalika.
Sera ya taifa ya ulemavu
inabainisha hali yan ulemavu kuwa ni, “kutokuwa au kupungukiwa na uwezo wa
kushiriki kwa usawa katika shughuli za kawaida
za kijamii kutokana na sababu za mapungufu ya kimwili, kiakili au kijamii”.
Sera hiiinatoa mwongozo wa kutolewa kwa
haki na fulsa sawa kwa walemavukupata mambona huduma za msingi kama elimu, taarifa, ajira, matunzo huduma za
afya, kumudu na kufikia huduma muhimu. Katika siku za karibuni kumeongezeka vitendo
vya kikatili dhidi ya albino ambavyo ni pamoja na mauaji ya kikatili na kukatwa
viungo kutokana na imani za kishirikina. Watu wenye ualbinowanalindwa kisheria
kutokana na vitendo hivi kwa kupitia sheria zilizopo za makosa ya jinai.
Serikali pia imechukua hatua za kudhibiti hali hii isiendelee kutokea ikiwa ni
pamoja na kuanza kuwaandikisha rasmi (kufanya sense) watu wenye ualbino, na pia
kuanzishwa kwa ulinzi kwa Albino kupitia jeshi la polisi na jamii kwa ujumla.
Mpaka sasa kunajitihada
zinazofanywa na serikali hasa katika utungwaji wa sera ila wakati Fulani kuna kulegalega katika
usimamizi wa sera hizo, kwa baadhi ya watu wasio waaminifu kuchukua muda mrefu
kufuatilia kesi hizi, ili hali kuna ushahidi pasipo shaka katika tuhuma hizo. Na
wengi wa watu wanaofanya vitendo hivi vya ukatili ni pamoja na baadhi ya wafanyabiashara vigogo, watu mashuhuri katika
jamii, na baadhi ya vigogo katika mamlaka, kwa imani potofu kuwa ili waendelee
kufanikiwa zaidi ni lazima wawapelekee hao waganga wa kienyeji baadhi ya viungo
vya watu wenye ulemavu wa ngozi. Ebu fikiria kidogo kwa akilia ya kawaida tu,
kwani yeye anayekwambia hivyo yeye hapendi kuwa na maisha mazuri?, mbona yeye
anaishi katika makaazi ya tope leo kesho linaanguka ? inamaana yeye hataki
kufanikiwa kimaisha?, baada ya kujiuliza maswali hayo tambua kuwa vitu vya
masharti ya kuleta viungo vya hawa albino mwisho wake ni kuitaka roho yako iwe
kama sadaka kwa miungu yao.
Wakati umefika sasa kama
ilivyofanywa kwa janga la ukimwi kwa kuanzisha mitaala mashuleni na vyuoni ,
pia ukatili huu wa kuwaua maalbino utangazwe kama janga la taifa na zichukuliwe
hatua mahususi na mbinu mbadala ili kukomesha tatizo hili, lakini pia kwa
upande wa jeshi la polisi nchini kuna baadhi ya watumishi wanaoshirikiana na
wahalifu hawa wa mauaji ya albino, kwa kupoteza ushahidi makusudi nao
wachukuliwe hatua pindi wanapobainika, maana tunaweza kuwaamasisha wananchi
katika mapambano haya ila ikaja kuonekana ni sawa na kumchezea mbuzi gitaa ili
acheze wakati hawezi kucheza muziki huo.
Tumeuanza mwaka mwingine tena ,
tena wenye purukushani nyingi kuelekea uchaguzi mkuu wa MADIWANI, WABUNGE NA
URAIS , BAADHI YAO WATATAPELIWA NA KUDANDANYWA KULETA VIUNGO VYA MAALBINO ILI
KUFANIKIWA KUINGIA MADARAKANI, Ukweli ni kwamba unajitengenezea laana wewe na familia yako isyokuwa na hatia, na kushindwa utashindwa tu. Haiwezekani kuiondoa roho ya mtu nawe ukabaki salama mbele za mwenyezi MUNGU.
No comments:
Post a Comment